Tuko Pamoja

Tuko Pamoja

Tuesday, August 20, 2013

Wenje mbaroni Mwanza

na Sitta Tumma, Mwanza
 
  Mbunge wa Nyamagana jijini Mwanza, Ezekiel Wenje (CHADEMA)
 
SIKU moja baada ya Jeshi la Polisi mkoani hapa kulazimika kutumia mabomu ya kutoa machozi kuwatawanya wananchi na wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), waliokuwa wakiandamana kutoka Uwanja wa Furahisha kuelekea Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, mbunge wa Nyamagana jijini Mwanza, Ezekiel Wenje (CHADEMA), amekamatwa akituhumiwa kutenda makosa mawili.
Wenje alishikiliwa jana majira ya saa 5 asubuhi kwa mahojiano na Jeshi la Polisi yaliyodumu takribani saa nne.
Mbunge huyo aliitwa polisi kwa ajili ya mahojiano kuhusiana na tuhuma za kuchochea maandamano na yeye kuandamana bila kibali, jambo lililosababisha ghasia na uvunjifu wa amani.
Inadaiwa na polisi kwamba mbunge huyo juzi aliongoza maandamano ya wafuasi wa CHADEMA na wananchi kutoka Uwanja wa Furahisha kuelekea ofisi ya mkuu wa mkoa, yalikokuwa yakifanyika mazungumzo baina ya Mkuu wa Mkoa Evarist Ndikilo na ujumbe ulioongozwa na mbunge wa Ilemela, Highness Kiwia kuhusu hatima ya meya, naibu wake, na madiwani watatu waliofukuzwa kinyume cha sheria.
Wenje aliyeongozana na mwanasheria wake, Charles Kiteja, baadhi ya madiwani wa Nyamagana na Ilemela na viongozi wa CHADEMA Kanda ya Ziwa Magharibi, alifika katika ofisi ya Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Mwanza (RCO), majira ya saa 5 asubuhi.Akiwa huko, RCO Joseph Konyo na baadhi ya maofisa wengine wa jeshi hilo, walitumia takribani dakika 45 wakimhoji mbunge huyo kuhusiana na tuhuma hizo dhidi yake.
Wenje ambaye anasifika kwa msimamo na ushawishi mkubwa kwa wananchi ndani na nje ya jimbo lake la Nyamagana, aliliambia gazeti hili kwamba: “Polisi wanadai nimewaambia wananchi kwamba Ndikilo na Matata ni adui wa wananchi, na wakiwaona wawazomee.
“Wananituhumu pia kuongoza waandamanaji kutoka viwanja hivyo vya Furahisha kisha kuelekea ofisi za mkuu wa mkoa, pamoja na kusababisha barabara ya Nera-Makongoro Mission kuzibwa kutokana na ghasia zilizoibuka.”
Alipoulizwa kuhusiana na kushikiliwa kwa mbunge huyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, na Naibu Kamishna wa jeshi hilo, Ernest Mangu alikiri Wenje kushikiliwa.
“Kweli mheshimiwa Wenje tumemshikilia kwa mahojiano. Anatuhumiwa mambo mawili ya kuchochea maandamano na yeye kuandamana bila kibali cha polisi.
“Tunataka mheshimiwa Wenje atueleze alipata wapi idhini ya kuandamana bila kibali, na aliandamana na akina nani. Asipotutajia alioandamana nao tutamng’ang’ania yeye hadi kieleweke,” alisema RPC Mangu.
Juzi majira ya alasiri, ziliibuka ghasia baada ya Jeshi la Polisi kulazimika kutumia mabomu ya machozi, kuwatawanya wafuasi wa CHADEMA.
Ghasia hizo zilitokea wakati wa maandamano ya chama hicho yaliyolenga kupinga uchaguzi ‘batili’ wa Meya wa Manispaa ya Ilemela, Henry Matata na Naibu wake, Swila Dede, pamoja na kupinga kufukuzwa madiwani watatu wa chama hicho kinyume cha taratibu, kanuni na sheria za nchi.
Madiwani waliofukuzwa na Matata kinyume cha sheria na kata zao kwenye mabano ni Abubakar Kapera (Nyamanoro), Malietha Chenyenge (Ilemela), na Dany Kahungu (Kirumba).

No comments:

Post a Comment