Tuko Pamoja

Tuko Pamoja

Monday, August 12, 2013

CHADEMA inamuondoa Kaburu Mweusi nchini? Iungwe Mkono!

na Bryceson Mathias
CHAMA cha Demokrasia na maendeleo (CHADEMA) kupitia kwa mwenyekiti wake, Freeman Mbowe, hivi karibuni kimewahakikishia watanzania kuwa kitafanya kila linalowezekana kurejesha mali zote za Taifa zilizouzwa kinyemela kwa mikataba mibovu.
Ni rai yangu, Kama wenye mapenzi mema na nchi hii wanaona viongozi na CHADEMA inafanya kazi ya kumuondoa Kaburu Mweusi nchini, ili watoto wetu, vijukuu, vitukuu waje kuwa na rasilimali endelevu, basi wapongezwe na kuungwa mkono.
Mbowe alidai kuwa, Mwalimu Julius Nyerere na viongozi wenzake walipigana kuwaondoa Makaburu weupe na hivyo CHADEMA nao sasa wanafanya kazi ngumu ya kumuondoa Kaburu weusi ili watoto wanaokuja waweze kufaidi rasilimali zilizopo nchini.
Mbowe alisema hayo akitembelea Kata za jimbo la Hai, akiwa na wabunge zaidi ya 11 wa Chadema toka majimbo mbalimbali na kuweka wazi kuwa, ili kufanikiwa vita hivyo, watahakikisha Katiba mpya inaweka wazi ulazima wa kuanika mikataba yote ya kiuchumi iliyoingiwa na serikali.
Kauli ya Mbowe, imepokewa kama kufutwa machozi ya wananchi wengi wanaopenda haki zao zilizopiganiwa na Nyerere zirejeshwe, wakifananisha na Wana Ndoa waliofiwa watoto, hivyo mke kuwa na Ujauzito wenye Uhakikika wa mtoto atakayeishi ni furaha kwao.
Mwenyekiti huyo ambaye ni Mbunge wa Hai na Kiongozi wa Upinzani Bungeni,  alitolea mfano wa shamba alilopewa mwekezaji anayezalisha sukari la TPC, akisema hakuna anayejua ni kiasi gani cha fedha kinachoingia serikalini wala kilichoandikwa kwenye mkataba huo.
Mbowe alidai Mwekezaji huyo alipatiwa eneo kubwa la shamba pamoja na maji, huku wananchi wa maeneo hayo wakitaabika kwa uhaba wa ardhi.
“Hatuwezi kuangalia mali yetu ikienda na wananchi wanataabika. Tukipata katiba mpya lazima mali zote zilizochukuliwa na wawekezaji mikataba irudiwe na iwekwe hadharani.
“Mkoa wa Kilimanjaro ulikuwa na viwanda vingi vilivyokuwa vinafanya kazi vizuri, lakini wamepewa wawekezaji ambao kwa sasa hakuna anayejua mkataba walioingia na serikali na viwanda vingi Moshi vimekufa,” alisema.Mbowe.
 
Mbowe aliwakumbusha watanzania Juhudi za Mwalimu Nyerere na kusema, Nyerere na  viongozi wenzake walipigana kuwaondoa Makaburu weupe na hivyo kuwa CHADEMA sasa nayo inafanya kazi ngumu kumuondoa Kaburu mweusi ili watoto wanaokuja waweze kufaidi rasilimali zilizopo nchini.
 
“Hivyo wananchi wangu wa Hai mkiniona niko kimya natafuta ukombozi wa nchi hii, baada ya kutoka hapa nitafanya mikutano nchi nzima, lakini ninawaahidi tukimaliza Bunge la Katiba lazima nije kushinda na nyie kusikiliza zaidi kero zenu,” alisema Mbowe.
 
Angalizo la Mbowe na Chama chake cha Chadema, litufumbuwe macho watanzania, kwa sababu ni ukweli usiopingika kwamba, viwanda vyote vya sukari nchi kikiwemo Mtibwa, Kilombero na Kagera, sasa hivi vimekuwa havina faida kwa wananchi na wafanyakazi wa  maeneo husika.
 
Yapo maeneo mengi ya uwekezaji, ambayo yana tatizo la mikataba mibovu inayodaiwa ni ya siri, ambayo licha wananchi kukosa maeneo ya kulima, lakini wanakosa hata haki za kupata maendeleo yao wenyewe kuhusiana na kuwepo kwa uwekezaji huo.
 
Pengine kwa tamko la CHADEMA na viongozi wake, limegusa mioyo ya watanzania, ambao kwa hapa nchini katika uwekezaji, wamekuwa watumwa wa wawekezaji katika nchi yao wenyewe, huku wakifanyizwa kazi utumwa kwa kipato duni, ndani ya rasilimali walizoziasisi wenyewe, huku faida ya kutisha ikisombwa na kusafirishwa kwenda nje.

No comments:

Post a Comment