Tuko Pamoja

Tuko Pamoja

Tuesday, August 31, 2010

Wabunge Mbeya wazomewa mbele ya Kikwete

 MGOMBEA urais kwa tiketi ya CCM, Jakaya Kikwete juzi aliendelea na mikutano yake ya kampeni katika mikoa ya Katavi, Rukwa na Mbeya ambapo katika mikutano yake wagombea ubunge walizomewa.Kikwete aliwasili mkoani Mbeya jana na kuanzia kampeni zake kwenye mji mdogo wa Tunduma ambao uko mpakani mwa Zambia na ambao una pilikapilika nyingi za wafanyabiashara wa Tanzania na nchi hiyo jirani.

Tofauti na mikutano mingine ya kampeni katika majimbo mbalimbali ambayo ameshatembelea kwenye kampeni zake, Kikwete alikumbana na hali isiyo ya kawaida wakati alipowanadi kwa nyakati tofauti wagombea hao wa majimbo ya Nkasi Kusini, Desderius Nipata na wa Mbozi Kusini, Lucas Siyame.
Tukio la kwanza la kuzomea lilitokea kwenye Uwanja wa Kate, ulio katika Kata ya Kate ambako wananchi walizomea baada ya mgombea wa Jimbo la Nkasi kuwataka wampigie kura KikweteLakini alipoanza kuomba wananchi hao wampigie kura na yeye ili afanye kazi na Kikwete, wananchi hao walianza kumzomea.

Mjini Mbozi tukio la mgombea ubunge kuzomewa lilimkumba Dk Lucas Siyame baada ya kuitwa jukwaani na Kikwete ili awasalimie wananchi baada ya kumaliza hotuba yake fupi kutokana na kuwa na mkutano mwingine kwenye mji mdogo wa Vwawa wilayani Mbozi ambao, hata hivyo, uliahirishwa hadi leo asubuhi."Sipo peke yangu, jamani nawaombea kura pia madiwani, na mbunge,’ alisema Kikwete lakini kauli hiyo ilipokewa na kelele za wananchi waliokuwa wakipiga kelele kusema “maji, maji, maji, hatutamtaki huyo.”
Wananchi hao walipiga mayowe hayo huku wakionyesha ishara ya vidole viwili ambayo ni alama ya Chadema, hali iliyomaanisha kuwa wanamuunga mkono mgombea wa chama hicho cha upinzani.
Upepo wa kisiasa kwenye mji huo haujaikalia vizuri CCM kutokana na hali ilivyojionyesha dhahiri kwenye mkutano huo. Wakati baadhi ya watu walionekana kumkubali Kikwete, wengine walikuwa wakipiga miluzi na baadhi kuonyesha ishara ya vidole viwili.

Baada ya Kikwete kumaliza hotuba yake, wananchi hao walipiga miruzi na kunyoosha mikono juu wakionyesha alama za vidole viwili kuashiria kuikubali Chadema.
Awali kulikuwa na dalili za wazi kumkubali Kikwete na kumpimnga Dk Siyame na wananchi wengi walitaka kuzungumza na wanahabari kueleza kero yao. Baadhi waliiambia Mwananchi kuwa wana shida kubwa ya maji pamoja na serikali kutoa zaidi ya Sh600 milioni kwa mradi wa maji, fedha walizodai zimeliwa huku mbunge huyo akikaa kimya.

Baadhi ya wananchi walisikika wakisema, kura zetu za ubunge tutampa wa upinzani. Huyu Siyame hajaonekana hapa tangu achaguliwe miaka mitano iliyopita,” alisema mmoja wa wakazi hao wa Mbozi.

No comments:

Post a Comment