Tuko Pamoja

Tuko Pamoja

Thursday, September 5, 2013

Mtei amvaa Kingunge


 Jaji Bomani naye amvutia pumzi
 
na Edson Kamukara

 
MUASISI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Edwin Mtei, amesema kauli ya Kingunge Ngombale - Mwiru kwamba wazee wanaounga mkono muundo wa muungano wa serikali tatu wamechanganyikiwa ni ya kutokujua hesabu.
Wakati Mtei akijibu mapigo hayo, mkongwe mwingine wa siasa nchini, Jaji mstaafu Mark Bomani, amesema kuwa anamvutia pumzi Kingunge hadi wiki ijayo.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Kingunge alizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake jijini Dar es Salaam na kuwashambulia wazee wenzake wanaounga mkono mapendekezo ya rasimu ya Katiba mpya ya kuwa na muundo wa serikali tatu kwamba ni sawa na watu waliochanganyikiwa.
Kingunge alifafanua kuwa anashangaa kuona wanaopendekeza muundo huo miongoni mwao ni wazee ambao walishiriki kuundwa kwa muungano uliopo mwaka 1964, ambao umeleta mafanikio kwa kujenga udugu na umoja wa kitafa.
Alisema baadhi ya viongozi wameshindwa kuthamini mafanikio ya muungano na hivi sasa mawazo yao yote wamekuwa wakiyaelekeza kwenye vyeo vyenye marupurupu.
Akizungumza na Tanzania Daima jana, Mtei ambaye pia ni Gavana mstaafu wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), alisema kuwa muundo wa sasa wa serikali mbili umeshindwa kuondoa kero za wananchi, hivyo ili kuondoa malalamiko lazima kwenda kwenye serikali tatu.
“Chama changu na mimi mwenyewe tunataka serikali tatu. Sasa Kingunge kama anasema sisi tumechanganyikiwa nadhani hajui hesabu hii nyepesi.
“Lazima tuwe na serikali tatu; ya Tangayika, Zanzibar na ile ya Muungano. Muundo huu wa serikali mbili ambao hata hivyo ni sawa na serikali moja ya Bara ambayo imeimeza Zanzibar umeshindwa,” alisema.
Mtei alifafanua kuwa chini ya muundo wa serikali mbili lawama na kero zimekuwa nyingi, hivyo katika kuondosha kero hizo lazima serikali ziwe tatu na baada ya hapo atakayetaka kujitenga aende afanye atakavyo bila kulazimishwa.
“Wengi wape, watu wanataka serikali tatu, hivyo lazima twende huko. Na wala hatuendi kupigania madaraka na vyeo kama anavyosema Kingunge, bali ni matakwa ya watu,” alisema.
Naye Jaji Bomani ambaye pia aliwahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati wa uongozi wa hayati Mwalimu Julius Nyerere, alisema kuwa kauli ya Kingunge ni nzito na hategemei kama alinukuliwa vibaya.
“Naomba univumilie nitazungumzia hilo pamoja na mambo mengine yanayopotoshwa wiki ijayo ili kuyaweka sawa,” alisema.
Kingunge katika mazungumzo yake hayo mbali na muundo wa serikali tatu pia alidai kuwa Chama chake Cha Mapinduzi (CCM) kilikurupuka kuanza mchakato wa Katiba mpya wakati haikuwa sera yao kwenye ilani ya 2010/2015.
Mkongwe huyo amewahi kuwa mshauri wa masuala ya kisiasa wa Rais Kikwete katika awamu ya kwanza ya utawala wake.
Alisema kuwa CCM haikukaa pamoja kama walivyofanya kwenye mchakato wa kuingia kwenye mfumo wa vyama vingi mwaka 1990.
Kauli yake hata hivyo imetafsiriwa kama ya kupingana na uamuzi wa Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, kwani licha ya suala hilo la Katiba mpya kutokuwamo kwenye ilani ya uchaguzi, aliafikiana na hoja ya wapinzani akakubali serikali yake ilifanyie kazi.
Kuhusu suala la uraia wa nchi mbili, Kingunge alisema lilikuwa linasemwa pembeni lakini sasa wanataka liingizwe kwenye Katiba.
“Mwanzo nilijua ni utani, lakini nilishangaa suala hili kubwa kuliona limeingizwa kwenye kijitabu kilichotolewa na chama changu na kupendekeza hivyo,” alisema.
Alisema suala la uraia ni la nchi, hivyo chama kilipaswa kutoa nafasi kwa wananchi kujadili kwa kina jambo hilo na si viongozi kujiamulia wenyewe.
Alisema amekuwa kwenye Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM kwa muda mrefu lakini hakuwahi kusikia hata siku moja suala hilo likijadiliwa, jambo alilodai ni hatari.

 

No comments:

Post a Comment