Tuko Pamoja

Tuko Pamoja

Thursday, September 5, 2013

Mbowe aibana polisi


na Salehe Mohamed
KIONGOZI wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe (CHADEMA) ameibana serikali ieleze ni lini itaunda tume huru ya kuchunguza matukio yanayosababishwa na mapambano kati ya askari na raia.
Mbowe alitoa kuali hiyo wakati akiuliza swali la nyongeza bungeni akihoji kwa nini askari wamekuwa wakienda na risasi na mabomu katika mikutano ya wananchi hasa ile ya CHADEMA.
“Matukio ya mapambano ya askari na raia sasa yameongezeka, hasa kwenye mikutano ya CHADEMA, tumeiomba serikali iunde tume huru kuchunguza jambo hili, ni nini kauli ya serikali kuhusu matukio hayo?” alihoji.
Akijibu maswali hayo, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereila Ame Silima, alisema kuwa askari wanakabidhiwa silaha za aina mbalimbali wanapokwenda kwenye mikusanyiko ya watu.
Silima alisema matumizi ya silaha hutumika kuanzia ngazi za chini na hupanda kadiri vurugu zinavyoongezeka.
Alisema polisi hulazimika kutumia risasi kwa wafanya vurugu wazoefu.
Aliongeza kuwa askari wamepata mafunzo ya kudhibiti vurugu na aina ya silaha zinazotumika kwenye mikusanyiko ya watu.
Waziri Silima alisema hali inapokuwa mbaya eneo la vurugu askari hulazimika kutumia silaha kubwa zaidi kama watu hawataki kutawanyika.
Alibainisha kuwa kwa kawaida jeshi hilo limekuwa likihimiza utii bila shuruti lakini inaposhindikana matumizi ya nguvu hayaepukiki.
Kuhusu kuundwa kwa tume huru, alisema mpaka sasa hakuna mahitaji hayo kwa kuwa jambo hilo linafanywa na polisi.
Aliongeza kuwa kama ukifika wakati tume hiyo itahitajika serikali haitasita kutekeleza jambo hilo.
Awali katika swali la msingi la Mbunge wa Jang’ombe, Hussein Mussa Mzee (CCM) alitaka kujua kama mabomu ya machozi yana madhara kwa binadamu.
Alitaka pia kujua kama polisi hawana mbinu au silaha nyingine wanazoweza kutumia ili kuepusha madhara yanayotokea katika mikusanyiko ya watu.
Akijibu maswali hayo, Silima alisema wananchi wanapaswa kujifunza kutii sheria bila shuruti ili kuepusha mapambano na askari.
Alibainisha kuwa mabomu ya machozi hayana madhara endelevu kwani silaha hizo zimefanyiwa uchunguzi wa kimaabara na kukubalika kimataifa.
Alisema silaha hizo zikitumiwa vizuri hazina madhara makubwa kwa binadamu zaidi ya kuwasha macho na athari hizo hudumu kwa muda mfupi tu.
Silima alisema kuna sheria za kitaifa na mikataba ya kimataifa inayoelezea matumizi ya nguvu za polisi katika kudhibiti vurugu.
Alisema kulinga na utendaji wa polisi na sheria hizo polisi hutumia silaha za aina nyingi zikiwamo virungu, maji ya kuwasha, risasi baridi, mabomu ya machozi, mbwa na farasi kwa kutegemea aina ya vurugu, wingi wa watu na aina ya silaha walizonazo.
Mwisho

No comments:

Post a Comment