Tuko Pamoja

Tuko Pamoja

Wednesday, June 29, 2011

Mbunge wa Mbeya Mjini akikagua mradi wa mabwawa ya samaki jijini Mbeya

Mh Joseph mbilinyi akisalimiana na wenyeji katika mradi huu wa ufugaji wa samaki


 Hapa akipata maelekezo kutoka kwa wataalam wa ufugaji samaki ambao wali sema  kwamba kwa bwawa lenye ukubwa huu ndani ya kipindi cha miezi mitatu na nusu bwawa hili lina uwezo wa kuzalisa tani saba mpaka tuni za samaki .

hatua ya kwanza ya  ujazaji wa maji ya  kuanzia yalipatikana katika mto ulio jirani na bwawa hili
                                                          ujazaji maji ukiendelea
 chanzo cha maji ambacho kitakuwa kikitumika kujaza maji katika bwawa baada ya hatua ya kwanza kukamilika

Tuesday, June 28, 2011

Tahadhari na kauli za Pinda kuhusu Katiba Mpya

Tarehe 25 na 26 Juni 2011 Vyombo mbalimbali vya habari vimemnukuu Waziri Mkuu Mizengo Pinda akitangaza kwamba katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itazinduliwa tarehe 26 Aprili 2014 katika maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano.
Kufuatia ahadi hiyo ya Waziri Mkuu, baadhi ya wananchi wa Ubungo na vyombo mbalimbali vya habari mmetaka kupata kauli yangu kuhusu tamko husika. Naomba kuwasilisha kwenu maoni yangu yafuatayo:

Pamoja na kutambua kwamba hatimaye Serikali imetangaza muda rasmi wa ukomo wa kukamilika kwa mchakato husika bado ahadi hiyo ya Waziri Mkuu Pinda inapaswa kupokelewa kwa tahadhari na anapaswa kutoa kauli ya kina bungeni itayoambatana na kuweka ratiba katika mipango, maazimio na sheria.

Hii ni kwa sababu katika Hotuba yake bungeni kuhusu mapitio na mwelekeo wa kazi za serikali na makadirio ya matumizi ya fedha ya ofisi ya Waziri Mkuu na ofisi ya Bunge ya mwaka 2011/2012 Waziri Mkuu Pinda hakueleza tarehe hiyo badala yake alitoa tu kauli ya ujumla kwamba “Serikali imejipanga kuhakikisha kwamba dhamira inatekelezwa ili nchi yetu iwe na katiba mpya kabla ya mwaka 2015”. Hivyo, ni muhimu ukomo huo wa Aprili 2014 kuwasilishwa rasmi bungeni kupitia kauli ya serikali au kupitia majumuisho ya hotuba ya Waziri Mkuu kabla ya mjadala wa muswada wa sheria na uzingatiwe katika mipango, maazimio na sheria.

Ikumbukwe kwamba tarehe 19 Disemba 2010 na 27 Disemba 2010 kupitia mikutano na wanahabari wakati nikieleza kusudio la kuwasilisha hoja binafsi kuhusu mchakato wa katiba mpya na kutoa taarifa ya hoja husika nilieleza bayana kwamba kati ya mambo ambayo yanapaswa kupangwa na bunge ni pamoja na muda wa mchakato wa katiba mpya; suala ambalo lisingezingatiwa katika mchakato uliotangazwa awali kufanywa na serikali bila kuanzia bungeni.

Nilieleza wasiwasi wa wadau mbalimbali kuwa ukomo wa muda usipowekwa kwa mujibu wa sheria ama maazimio ya bunge, serikali inaweza kuchelewesha mchakato mzima kwa kutoa visingizio mbalimbali ili usikamilike mapema kuwezesha maandalizi ya kisheria na kitaasisi kufanyika kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kwa kutumia katiba mpya.
Aidha umma unapaswa kuipokea ahadi hiyo ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliyoitoa kupitia Semina Elekezi kwa wakuu wa mikoa, wilaya na makatibu tawala wa mikoa kwa tahadhari kwa kuwa imeambatana na kauli tata kuhusu mchakato mathalani serikali kutokuwa na uhakika kuhusu wakati ambapo muswada wa sheria ya mapitio ya sheria ya marekebisho ya katiba wa mwaka 2011 utawasilishwa bungeni.

Waziri Mkuu Pinda amenukuliwa akisema kwamba muswada huo utawasilishwa bungeni mwishoni mwa mkutano wa nne wa Bunge unaoendelea hivi sasa au mwanzoni mwa mkutano wa tano wa bunge utakaofanyika Oktoba 2011; wakati katika mkutano wa tatu wa bunge Waziri Mkuu aliahidi kwamba muswada huo utarejeshwa katika mkutano wa nne wa bunge.
Ikumbukwe kwamba tarehe 30 Machi 2011 nilitoa tamko la kueleza kushtushwa na maudhui ya muswada wa sheria ya mabadiliko ya katiba wa mwaka 2011 (The Constitutional Review Act 2011) uliochapwa katika gazeti la serikali toleo No. 1 Vol. 92 la tarehe 11 Machi 2011.

Nilieleza kwamba maudhui ya muswada huo yamedhihirisha tahadhari niliyotoa mara kadhaa kwamba serikali haina dhamira ya kweli ya kuhakikisha panakuwepo na mchakato mzuri wa kuwa na katiba mpya; matokeo yake ni muswada huo uliowasilishwa kwa hati ya dharura kuondolewa katika ratiba ya kupitishwa katika mkutano wa tatu wa bunge kutokana na shinikizo la wadau mbalimbali. Hivyo, Waziri Mkuu Pinda anapaswa kutoa kauli bungeni kueleza bayana iwapo hati ya dharura ya muswada huo ilifutwa basi muswada husika uwasilishwe kwa kufuata taratibu za kawaida kwa mujibu wa kanuni za bunge.

Pia, umma unapaswa kuipokea kwa tahadhari ahadi hiyo ya Waziri Mkuu kwa kuwa imeambatana na kutolewa kwa maelekezo kwa wakuu wa mikoa, wilaya na makatibu tawala kuhusu maudhui ya mchakato wa katiba na kipi kinakusudiwa kufanywa na serikali wakati ambapo bado sheria haijapitishwa na bunge.

Maelekezo hayo ya Waziri Mkuu Pinda yanadhihirisha kwamba tayari serikali imeshachukua msimamo kuhusu mchakato utakaotumiwa kuandika katiba mpya hiyo; hali inayoashiria kuwa serikali ina dhamira ya kulitumia bunge kama muhuri (rubber stamp) ya kupitisha mchakato ambao tayari ulishapitishwa ndani ya serikali na maelekezo ya utekelezaji kuanza kutolewa kwa watendaji wa serikali ngazi ya chini kabla ya sheria kupitishwa.

Ikumbukwe kwamba tarehe 30 Machi 2011 nilitahadharisha kwamba muswada uliowasilishwa bungeni umelenga kuhalalisha yote ambayo yalitangazwa kufanywa na Rais kuhusu mchakato wa katiba mpya na kupingwa na wadau mbalimbali na yanataka kupewa uhalali kwa sheria inayotaka kutungwa na bunge kupitia muswada huo; mchakato ambao Waziri Mkuu Pinda ameurejea katika hotuba yake.

Kadhalika umma unapaswa kuipokea ahadi hiyo ya Waziri Mkuu Pinda kwa tahadhari kubwa kwa kuwa imeambatana na maelekezo ya kuwataka wakuu wa mikoa na wilaya wawe mstari wa mbele kuongoza mchakato huo wakati inaeleweka wazi kwamba wadau mbalimbali wamelalamikia mamlaka waliyopewa watendaji wa serikali katika mikutano ya kukusanya maoni kuhusu katiba kwa mujibu wa muswada uliowasilishwa awali ambao wananchi walitaka vifungu husika vibadilishwe.

Ikumbukwe kwamba watendaji hao wamelalamikiwa kwa miaka kadhaa kutumia madaraka yao vibaya ikiwemo kudhibiti uhuru wa wananchi katika kutoa maoni kwenye tume mbalimbali ambazo zimewahi kuundwa na serikali nyakati za nyuma kwa masuala mbalimbali ikiwemo yanayohusiana na marekebisho ya katiba. Aidha kati ya mambo ambayo wananchi wameanza kuyatolea maoni kwenye maudhui ya katiba ni pamoja na kutaka kufutwa au kupunguzwa mamlaka ya wakuu wa mikoa na wilaya; hivyo kitendo cha kuwaweka mstari wa mbele katika mchakato ni dalili za serikali kutokuwa na dhamira ya kweli ya kutaka mabadiliko ya katiba.

Katika muktadha huo; na kwa kuwa serikali ilishawasilisha awali muswada wa katiba natoa mwito kwa Spika na Ofisi ya Bunge kuhakikisha kwamba bunge linachukua nafasi yake kuanzia hatua za msingi kuhakikisha suala hili la mchakato wa katiba mpya lipata uhalali wa umma kwa kurejea ibara 8 ambayo inatamka kwamba madaraka na mamlaka ni umma serikali inafanya kazi kwa niaba na Bunge ndicho chombo kikuu cha kusimamia wajibu huo kwa kutokana na mamlaka ya kikatiba yaliyopo kwenye ibara ya 63(2) na (3) yanayohusu kutunga sheria na ibara ya 98 inayohusika na mabadiliko ya katiba.

Hivyo, badala ya kusubiri mpaka mwishoni mwa mkutano huu wa bunge tarehe 29 mpaka 30 Agosti 2011 ndipo wabunge wapewe tena muswada wa mabadiliko ya katiba pamoja na marekebisho yake yaliyofanyika ikiwemo tafsiri katika lugha ya Kiswahili; utaratibu wa kikanuni ufanyike kuhakikisha taarifa ya serikali inatolewa mapema pamoja na muswada huo nyeti.

Kwa upande mwingine umma unapaswa kuzipokea kwa tahadhari kauli za Waziri Mkuu Pinda kuhusu mchakato wa katiba mpya kwa kurejea msimamo wa wake wa awali kuhusu mabadiliko ya katiba alioutoa wakati akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari tarehe 17 Disemba 2010 ulikuwa na kumshauri Rais aunde jopo shirikishi ili kuratibu na kusimamia mchakato husika.

Izingatiwe kuwa tarehe 9 Februari 2011 nilitoa tamko la kupokea kwa tahadhari uamuzi wa Serikali kupitia kwa Rais Jakaya Kikwete na Waziri Mkuu Mizengo Pinda kubadili misimamo ya awali kuhusu mchakato wa katiba mpya na kuamua kukubaliana na mwito wa kutaka mchakato husika uanzie bungeni kupitia kutungwa kwa sheria ya bunge ya kuratibu na kusimamia mchakato husika kwa kuwa maneno ya kauli zilizotolewa hayaambatani na vitendo vya dhati vya kuweka mchakato mzuri wa katiba mpya.

Uthibitisho wa mwelekeo huo ni kwamba Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano (2011/2012-2015/2016) uliotiwa saini na Rais Kikwete tarehe 7 Juni 2011 haukuweka kipaumbele haja ya katiba mpya kwenye eneo la utawala bora na utawala wa sheria. Aidha, bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2011/2012 haikuweka bayana na kwa kiwango cha kutosha rasilimali kwa ajili ya mchakato wa katiba mpya suala ambalo pamoja na maelezo ya Waziri wa Fedha wakati wa kuhitimisha hoja bado serikali ina wajibu wa kulitolea ufafanuzi wa kina katika mkutano wa Bunge unaoendelea.

kwa hisani ya

John Mnyika (Mb)

Saturday, June 18, 2011

Wabunge, waziri watunishiana misuli

* Ni Kabaka, Jenista Mhagama, Mbilinyi (Sugu)
* Wavutana katika kutembelea kiwanda
* Kiwandani wabunge washuhudia ‘madudu’
* Wafanyakazi wanalazimishwa kuvaa kaptura
* Wabunge watokwa machozi kwa waliyoyaona


Na Arodia Peter
Dar es Salaam


WAZIRI wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana Gaudensia Kabaka jana alivutana vikali na wabunge wa Kamati ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii waliokuwa wanataka kutembelea Kiwanda cha Vyombo vya Nyumbani cha Jambo Plastiki kilichoko Dar es Salaam.
Wakati wajumbe wa Kamati hiyo wakiwa wamekwisha kujiandaa kwenda katika kiwanda hicho jana, ghafla Waziri Kabaka aliwaeleza kuwa ziara hiyo imeahirishwa hadi wakati mwingine.
Kabaka alitoa sababu za kutaka kuahirisha ziara hiyo kuwa ni mgogoro wa wafanyakazi na mwajiri kiwandani hapo ambao upo mahakamani hivyo ziara hiyo itakuwa ni kuingilia uhuru wa mahakama.
Baada ya kutolewa taarifa hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Jenista Mhagama alikuja juu na kumweleza Kabaka kuwa kamwe kamati yake haiwezi kuahirisha ziara hiyo bila kutolewa sababu za kuridhisha. Alisema kitendo alichokifanya Waziri kinadhalilisha kamati yake.
“Mheshimiwa Waziri kitendo ulichokifanya unaingiza mgogoro mkubwa katika kamati ya Bunge… kwa mazingira ya sasa Watanzania hawana mahali popote pa kutolea shida zao zaidi ya bunge na hii inadhihirika wazi wataalamu wako hawakukushauri vizuri,” alisema Mbunge huyo wa Peramiho kwa tiketi ya CCM na kuongeza:
“Basi kama ni hivyo, Mheshimiwa Waziri mimi nakupisha uwe mwenyekiti wa kamati ya Bunge maana naona hutaki kutuelewa.”
Kuona hivyo, Mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde alikwenda mbali zaidi kwa kusema kwa uzoefu uliopo nchini unaonyesha kuwa ziara hiyo tayari imekwicha kuchakachuliwa na wahusika kwa manufaa wanayoyajua wao.
Alisisitiza kwamba kama ziara itaahirishwa basi yeye hatakuwamo kwenye orodha hiyo.
Naye Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi (Chadema) alisema kama kamati haitaki kwenda kwenye kiwanda hicho yeye atapanga ziara yake kama mbunge wa Chadema na kwenda kusikiliza na kukagua mazingira kiwandani hapo.
Asumpta Nshunju (CCM) ambaye ni Mbunge wa Nkenge, alisema kuna dalili za wazi watu wamepokea chochote kutoka kwa mwekezaji ndiyo maana kamati imepigwa ‘stop’ dakika za mwisho.
Akimsaidia waziri wake, Ofisa Kazi Mfawidhi wa Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Josephat Rugakingira aliwaambia wabunge kwamba haingekuwa vizuri kutembelea kiwanda hicho wakati mgogoro kati ya menejimenti na wafanyakazi bado uko Baraza la Usuluhishi wa Migogogro (CMA) ikiwa imefunguliwa kesi namba DMA/DSM/ILALA/ 2009.
Hata hivyo baada ya mvutano mkali hatimaye Waziri Kabaka alikubaliana na wabunge na kuamua kufanya ziara kiwandani hapo wakati huo ikiwa saa 7.00 mchana.
Kiwandani
Wabunge walipofika kiwandani walipangua ratiba iliyokuwa imeandaliwa iliyotaka wafanyakazi na menejimenti kukutana na kamati ya Bunge kwa pamoja.
Kamati ya Bunge iliamua kukutana na wafanyakazi pekee, kikao kilichodumu kwa zaidi ya saa moja. Waandishi wa habari wa menejimenti hawakuruhusiwa katika kikao hicho.
Baada ya kumalizika kikao hicho, wabunge walitoka nje wakiwa wanafuta machozi na baadhi yao walisema waliingiwa na simanzi kubwa kutokana na mambo mazito waliyoelezwa katika kikao hicho.
Hata hivyo, ilibainika kuwa katika kikao hicho ambacho Waziri pia alishiriki, kesi iliyokuwa inasemwa kuwa ipo mahakamani haikuwa kweli kwa vile ilikwisha kutolewa uamuzi tangu mwaka 2009.
“Hii kama siyo rushwa ni nini, ndiyo maana walitaka kutuchakachua tusije hapa kwa maslahi yao, hii ni aibu. Wataalamu wa Wizara ndiyo wanaotufanya sisi wabunge wa CCM tuonekane hatuna thamani mbele ya umma… kumbe ni watu wachache waliojiwekea mtandao wa rushwa kwa njia wanazozijua wao,” alisema mmoja wa wabunge kwa sharti la kutotajwa jina.
Waziri Kabaka akiri, aiomba radhi kamati
Baadaye Waziri Kabaka aliomba radhi kwa Kamati ya Bunge kutokana na hali iliyojitokeza awali. Alisema yeye hakujua kama alichoambiwa na wataalamu wa Wizara yake kilikuwa ni uongo na uzushi.
“Mheshimiwa mwenyekiti naomba radhi kwa yaliyotokea, nakiri nilidanganywa sasa nimejifunza kutoka kwenu,” alisema Kabaka kwa sauti ya upole.
Alipoulizwa na waandishi wa habari ni hatua gani atawachukulia wataalamu waliomdang’anya, alisema:
“Niachieni nitashughulika nao, tutaongea na wenzangu tuone ni kwa nini wamefanya hivyo”.
Wafanyakazi wanalazimishwa kuvaa kaptura
Kiwandani hapo wabunge walishuhudia wafanyakazi wakike na kiume wakiwa wamevaa kaptura na fulana ikiwa ndiyo sare za kiwanda hicho.
Wakizungumzia hali hiyo baadhi ya wafanyakazi walisema hawaruhusiwi kuvaa nguo tofauti na hizo kiasi kwamba wakati wa baridi wanapata shidakubwa lakini hawana la kufanya.
“Hizi ndiyo nguo zetu rasmi hapa kazini. Tukivaa tofauti na hizi tunafukuzwa kazi, tunashukuru mmekuja wabunge wetu mtutetee tunaangamia,” alisema mmoja wa wafanyakazi hao.
Kwenye mgahawa wa wafanyakazi, hali pia ni mbaya na wabunge walishuhudia uchafu uliokithiri huku vyombo vya kulia chakula vikiwa vya plastiki jambo ambalo ni hatari kwa afya za wafanyakazi hao.
Baadhi ya wafanyakazi walisema licha ya kutumia vyombo vya plastiki pia wanalazimika kutumia vikombe kwa kupokezana kwa vile vilivyopo havitoshi.
“Hata sisi tunaonekana kana mbwa, angalieni sehemu hii tunayolia chakula. Haifai hata kwa mnyama mbwa maana ni chafu kupindukia lakini hawatujali,” walisema baadhi ya wafanyakazi.
Wafanyakazi wa kigeni
Mkurugenzi wa Kiwanda hicho, Manoj Suchak aliulizwa kuhusu hatua ya kuajiri wafanyakazi wa kigeni katika nafasi zote za juu bila kuhusisha mfanyakazi mzawa hata mmoja.
Akijibu swali hilo lililoulizwa na Mbunge wa Kondoa Kusini, Juma Nkamia (CCM), alisema kati ya mameneja saba wa kiwanda hicho ni watano tu ambao ni wazawa.
Hata hivyo Nkamia alipotaka amwone angalau mmoja ambaye ni mzawa, alitokea kijana mwenye asili ya Asia, jambo lililozua kicheko na miguno kutoka kwa wabunge.
Ziara hiyo ya wabunge ilikuwa pamoja na mambo mengine kukagua mazingira ya kiwanda, kusikiliza mgogoro baina ya wafanyakazi na manejimenti ya kiwanda hicho ambao umedumu kwa muda mrefu.