Tuko Pamoja

Tuko Pamoja

Saturday, April 9, 2011

NI MIMI NA HARAKATI NI ZILEZILE SEMA TUMEONGEZA UWANJA

Studio ya JK yazua mjadala bungeni


na Bakari Kimwanga, Dodoma

MBUNGE wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi (CHADEMA), jana iliibuka bungeni na kudai studio iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete kwa ajili ya kukuza vipaji kwa wasanii nchini wamepewa watu ambao hawana msaada kwa wasanii na hata chombo kinachoisimamia hakijasajiliwa.
Akiuliza swali la nyongeza baada ya lile la msingi la Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Martha Mlata, aliyetaka kujua wasanii wamenufaikaje na mtambo huo wa studio uliotolewa na Rais Kikwete, Mbilinyi maarufu kama ‘Mr II au Sugu’, alihoji kutokana na hali hiyo kwa nini serikali imekuwa inapata kigugumizi kulipa mamlaka Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) ili kuiendesha kikiwa ni chombo ambacho kinasimamia maslahi ya wasanii wote nchini.
“Mheshimiwa Spika ninazungumza kwa niaba ya wasanii wa hapa nchini, hakika hiki chombo kinachoitwa Tanzania Flava Unit hakijasajiliwa na hata BASATA waligoma kukisajili kutokana na kazi zake kufanana na Chama cha Wanamuziki wa Muziki wa Kizazi Kipya nchini, sasa serikali haioni haja ya kuipa BASATA kusimamia studio hii?” alihoji Sugu.
Aidha aliongeza kuwa kutokana na hali hiyo, kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wasanii nchini kuhusu studio hiyo kutowasaidia na hata kushindwa kurekodi nyimbo zao.
Swali hilo lilimuinua Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Emmanuel Nchimbi, ambapo alijibua kuwa hakuna sheria inayozuia kusajiliwa kwa Tanzania Flava Unit kama kazi ya kusimamia studio hiyo iko sahihi, huku Baraza la Sanaa akiahidi kutafutiwa kazi nyingine.
Awali akijibu swali la msingi, Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, alisema, ‘Mastering Studio’ iliyotolewa na rais, haikutolewa kwa kituo cha radio cha Clouds FM, bali imetolewa kwa kikundi cha wasanii waliojiunga pamoja na kuanzisha Chama cha Tanzania Flava Unit.
Alisema wasanii hao ni wale wa Tanzania House of Talent (THT), na baadhi ya wanamuziki wa kizazi kipya ambao wana ushirikiano wa karibu sana wa kiutendaji kazi na kituo cha Radio Clouds FM kinachoongozwa na Ruge Mutahaba na bado haijaanza kufanya kazi, hivyo ni mapema kueleza ni wasanii wangapi wamenufaika.

Wednesday, April 6, 2011

Mbunge Joseph Mbilinyi apinga kiwanda kugeuzwa ghala la bia.

Na Joachim
Nyambo,Mbeya

MBUNGE wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi, maarufu kama Mr II, amesema
kitendo cha serikali mkoani hapa kukabidhi majengo ya kilichokuwa
kiwanda cha zana za kilimo (ZZK) yaliyopo eneo la Iyunga jijini hapa
kwa kampuni ya vinywaji ya TBL yatumike kama maghala kinakinzana na
mpango wa serikali wa kufufua viwanda muhimu kama hicho.

Mhe. Joseph Mbilinyi (Sugu) akiwa katika moja ya mikutano yake

Kabla ya kusimamisha uzalishaji wa zana zaidi ya miaka kumi iliyopita
hali iliyosababishwa na mwekezaji aliyekabidhiwa kushindwa kukiendesha
kiwanda hicho kilikuwa tegemeo kubwa la wananchi wa mkoa wa Mbeya
ambao asilimia yao kubwea ni wakulima.
Akizungumza na mamia ya wakazi wa kata za Nsalaga na Uyole  katika
viwanja vya kibonde Nyasi, Mbunge huyo amesema hatua hiyo moja kwa
moja imewapa hofu wananchi kuwa huenda serikali haina mpango tena wa
kukifufua ili kiendelee na uzalishaji wa zana hizo ambao utaweza
kuwapunguzuia gharama za ununuzi wa pembejeo tofauti na ilivyo hivi
sasa.
Amesema  inashangaza kuona kuwa baadhi ya watendaji wa serikali ambayo
kila siku inahubiri mpango wa kukuza uchumi wa wananchi wake kupitia
kilimo kwa sera mbalimbali ikiwemo Kilimo Kwanza wanakubali kumpa
mwekezaji ambaye anayegeuza kiwanda cha ZZK kuwa ghala la kuhifadhia
bia.
Amesema wananchi wa mkoa wa Mbeya kwa ujumla walikitegemea sana
kiwanda hicho kiweze kufufuliwa na kuzalisha zana za kilimo ambazo
zingepatikana kwa urahisi kwani zingeuzwa kwa bei ndogo kwa wakulima
ili waweze kuboresha kilimo chao lakini sasa matumaini yao yameanza
kufifia.
Mbilinyi amesema kama kiwanda hicho kingefufuliwa hata Trekta ndogo
aina ya Powertiller zinazoagizwa nje ya nchi kwa bei kubwa zingeweza
kuzalishwa katika kiwanda hicho na kuuzwa kwa bei ambayo wakulima
wangemudu kununua.
Hata hivyo Mbilinyi amesema yupo tayari kubisha hodi katika ofizi za
Waziri wa Viwanda ili apewe maelezo ya kina juu ya mwongozo uliotumika
kwa serikali kugeuza kiwanda hicho kuwa ghala la kuhifadhia bia badala
ya kuweka mikakati ya kukifufua.
Aidha Mbunge huyo amepongeza hatua ya seriakali kujenga uwanja wa
ndege wa Songwe , akisema ameridhishwa hatua za ujenzi zinazoendelea
baada ya kuutembelea na kuelezwa na wataalamu kuwa ifikapo Agosti
mwaka huu ndege zitakuwa zimeanza kutua katika uwanja huo.
Mbilinyi amesema kukamilika kwa uwanja huo ni changamoto kubwa ya
maendeleo katika mkoa wa Mbeya na kuwataka wananchi kujiandaa vyema
kuutumia uwanja huo kwa manufaa hususani kwa kuzalisha mazao
yanayoweza kusafirishwa nje ya nchi na kuuzwa kwa bei yenye kuwaletea
tija.

Siku Mhe. Joseph Mbilinyi Alipotembelea Jukwaa La Sanaa

Mbunge wa Mbeya Mjini Mh. Joseph Mbilinyi maarufu kwa Jina la Sugu akiongea na wadau wa Jukwaa la Sanaa jana wakati alipohudhuria kwa mara ya kwanza toka achaguliwe kuwa mbunge. Sugu ni moja ya wadau wa Jukwaa hilo linalofanyika kila Jumatatu Ukumbi wa BASATA.
 
Profesa Amandina Lihamba kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam akichokoza mada kuhusu tasnia ya Filamu hapa nchini kwenye Jukwaa la Sanaa BASATA jana. Kulia kwake ni Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego.

Na Mwandishi Wetu:
Jukwaa la Sanaa BASATA limempongeza kwa ushindi wa ubunge na kumpa kazi ya kutetea maslahi ya wasanii Mbunge wa Mbeya Mjini ambaye pia ni mmoja wa waasisi wa muziki wa kizazi kipya hapa nchini Joseph Mbilinyi maarufu kwa jina Sugu.


Akizungumza kwenye Jukwaa la Sanaa linalofanyika kila Jumatatu kwenye ukumbi wa BASATA kwa niaba ya wadau wote. Profesa Amandina Lihamba kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambaye alikuwa ni Mratibu wa Jukwaa hilo alisema kwamba, wadau wa Jukwaa la Sanaa wanampongeza kwa dhati kwa ushindi wake na wanamtuma bungeni kutetea haki zao na kwamba asiwatupe.


“Tunajua toka ushinde leo ni mara yako ya kwanza kuonana na hadhira ya wasanii hivyo tunachukua fursa hii kukupongeza kwa dhati, uendelee na moyo huo huo wa kuwapigania wasanii na usiwatupe” aliongeza Profesa Lihamba.


Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego alisema kwamba, pamoja na BASATA awali kutuma barua ya pongezi kwake na kwa wabunge wengine wasanii, bado Jukwaa la Sanaa lina kila sababu ya kumpongeza na kumtuma kwenda kutetea haki za wasanii na kuhakikisha maslahi ya sekta ya sanaa yanalindwa.


“Naomba niungane na wenzangu kutambua uwepo wa Joseph Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini, msanii mwenzetu naimani sasa tunapozungumza hapa katika Jukwaa tunazungumza na mtu ambaye sasa atakuwa bungeni akiwakilisha wasanii. Pamoja na barua ya kumpongeza tuliyomtumia yeye na wasanii wengine walioingia bungeni, tunampongeza tena kwa dhati” alisema Materego.


Naye Mbilinyi aliyeambatana na Katibu wake Fred Maliki, maarufu kwa jina la usanii la Mkoloni alimshukuru Materego kwa pongezi zake lakini akapongeza juhudi anazochukua katika kuwahabarisha na kuwapa fursa ya elimu wadau wa sanaa. Aliahidi kuendeleza harakati za kupigania haki za wasanii kwani ndicho kitu ambacho ataanza nacho.


“Harakati za kupigania haki za wasanii nimezianza kwa muda mrefu nawaahidi kwamba sitarudi nyuma na kwa sasa napenda niwaambie kwamba, mapambano ndiyo kwanza yameanza kwani sasa ndiyo tumekabidhiwa rungu” alimalizia Mbilinyi ambaye aliwahi kutamba na nyimbo kama za Mikononi mwa polisi, Deiwaka, Dar moto chini, Wananiita Sugu, Hold On na nyingine nyingi.

Mr II ajisifu kwa kuweka historia bungeni

MBUNGE wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Mr II au Sugu’ ametamba na kujifafanisha na Spika wa Bunge, Anne Makinda katika kuweka historia ya yeye kuwa msanii wa kwanza wa muziki wa bongo flava kuingia bungeni kama ilivyo kwa Spika ambaye ni mwanamke wa kwanza kuongoza Bunge.

Mbilinyi, ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni, alitoa majigambo hayo jana wakati akisoma maoni ya Kambi ya Upinzani kuhusu Azimio la Serikali la Kuridhia Mkataba wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) la Kulinda Urithi wa Utamaduni Usioshikika wa mwaka 2003.
Mh Joseph Mbilinyi a.k.a Mr II akipongezwa na Spika wa Bunge Mh Anna Makinda

Azimio hilo liliwasilishwa jana bungeni na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk Emmanuel Nchimbi. Kabla ya kutoa maoni hayo, Mbilinyi alisema, “Kwa heshima kubwa niwashukuru wananchi wa Mbeya Mjini kuniwezesha kuweka historia ya kuwa msanii wa kwanza wa Bongo Flava kuchaguliwa kuwa Mbunge, Mheshimiwa Spika, mimi na wewe tumeingia katika historia kupitia Bunge hili la kumi, kwa mimi kuwa msanii wa kwanza wa Bongo Flava kuingia bungeni na wewe kuwa Spika wa kwanza mwanamke kuliongoza Bunge,” alisema Mbilinyi na kufanya wabunge kuangua kicheko.

Mbilinyi baada ya kueleza kuwa suala hilo ni la kihistoria na yeye anafarijika ameingia katika historia, alimpongeza Makinda na kuendelea kutoa maoni ya kambi ya upinzani yaliyounga mkono hoja hiyo na kueleza kuwa azimio linalenga kulinda hadhi ya Mtanzania.

Baada ya maoni ya Kambi hiyo ya Upinzani, baadhi ya Wabunge walipata fursa ya kuchangia azimio akiwemo msanii mwingine, Mbunge wa Viti Maalum, Vick Kamata (CCM) ambaye aliunga mkono hoja na kueleza kuwa mkataba huo ukiridhiwa utawawezesha wasanii kutambulika kimataifa na kazi zao kuweza kulindwa kwa kuwa suala la hatimiliki limezingatiwa kwa upana katika mkataba huo.

Naye Mbunge wa Peramiho, Jenista Mhagama (CCM) alisema kilio cha wasanii wa nyimbo za asili zinazobeba utamaduni wa Kitanzania, kimefika mahali pake na kutaka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa, kupigwe nyimbo za asili za makabila yetu badala ya nyimbo za kigeni zinazopigwa hivi sasa.